Rais JPM asimamisha bomoa bomoa ya nyumba zaidi 17,000 Dar - TANZA MEDIA ONLINE

Friday 1 September 2017

Rais JPM asimamisha bomoa bomoa ya nyumba zaidi 17,000 Dar



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Dkt. John Pombe Magufuli amesitisha zoezi la bomoa bomoa kwa Nyumba zaidi ya elfu kumi na saba (17, 000) zilizotangazwa kubomolewa na Baraza la Hifadhi ya Mazingira NEMC.

Hatua ya kusitisha zoezi hilo, Imekuja kufuatia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Paul Makonda kuzungumza na Mhe Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kuhusiana na Sintofahamu ya bomoa bomoa hiyo ambayo amemueleza Mhe Rais Magufuli kuwa Taarifa za bomoa bomoa ya Nyumba elfu kumi na saba iliyotolewa haikufika ofisini Kwake Jambo ambalo ni tofauti na Taratibu za Utendaji kazi wa Serikali.

Mhe Makonda amesema, hata kama tamko hilo limetolewa na watumishi wa Mkoa mfano Wakurugenzi wa Manispaa au Wakuu wa Wilaya walioko Chini ya Mamlaka ya Mkuu wa Mkoa lazima Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ipate taarifa n iruhusu bomoa bomoa hiyo, na pia hata kama taarifa zimetoka wizarani inapaswa taratibu za kimaandishi zifuatwe kwa kujulisha Ofisi ya Mkoa.
“Haiwezekani mtu kutoa tamko la kuvunja nyumba elfu kumi na saba bila mkoa kujua, hilo haliwezekani,” amesema Mhe Makonda.

Makonda amefafanua kuwa ameongea na Mhe Rais Magufuli na Kumuuliza kama ana taarifa za zoezi la Ubomoaji wa Nyumba elfu kumi na saba ambapo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Paul Makonda alimueleza Mhe Rais Magufuli kuwa hana taarifa hizo za ubomoaji, zaidi Ubomoaji wa Nyumba zilizo kwenye Hifadhi ya Barabara ya kuanzia Ubungo kwenda Kimara na Mbezi ubomoaji unaofanywa kwa ajili ya upanuzi wa Barabara ya Morogoro, Ubomoaji wa Nyumba zilizo Jirani na reli hususani ni zile zinazohusiana na Ujenzi wa Reli Mpya na ya Kisasa.

Kutokana na sababu hizo, Makonda amesema Rais amesikitishwa na tamko hilo la kutaka kubomolewa kwa nyumba zaidi ya elfu kumi na saba na ametoa pole kwa wananchi waliokumbwa na taharuki na tamko hilo la Ubomoaji, na kusisitiza kuwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli hakuchaguliwa kwa ajili ya kubomoa nyumba za watu na kusisitiza kuwa anataka wananchi wanaoishi katika maeneo halali kuachwa maana amepata taarifa kuwa huenda zoezi hilo lingekwenda mbali zaidi mpaka kwa wananchi wasiohusika.

Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda amepiga marufuku zoezi lolote ubomoaji wa nyumba pasipo ofisi yake kupewa taarifa na kisha kuridhia ubomoaji huo.
Mwisho, Paul Makonda amewataka wananchi na wakazi wote wa Mkoa wa Dar es Salaam kuzingatia sheria na wasivamie maeneo au kuuziwa viwanja na matapeli na pia amewataka wananchi kuchukua tahadhari hususani ni katika maeneo yote hatarishi ambayo sio salama kwa wakazi na kuwataka kila mwananchi mwenye familia kutafuta salama kwa maisha yake na ya familia yake.

Makonda pia ametoa ombi Maalumu Kwa Waziri Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe William Lukuvi la kuboresha mfumo wa Ardhi katika Mkoa wa Dar es Salaam kwa kuanzisha mpango wa kuweka maafisa ardhi katika kata zote za Mkoa wa Dar es Salaam ambao watakuwa na jukumu la kusimamia, kuratibu masuala yote ya Ardhi ngazi ya kata hatua ambayo itasaidia kuondoa Migogoro na utapeli kwa Wananchi kuuziwa au kununua Ardhi katika maeneo ambayo hayaruhusiwi.

Amesema amepata wazo hilo kutokana na uzoefu aliopata akiwa Rais wa umoja wa Vyuo Vikuu (TAHILISO) ambapo alishirikiana na Bodi ya Mikopo kuanzisha mfumo wa kuwa na maafisa mikopo katika vyuo hatua iliyosababisha kuondoa kero ya wanafunzi kufuatilia Mikopo katika Ofisi za bodi ya Mikopo hatua ambayo imekuwa mwarobaini wa tatizo la kufuatilia Mikopo kwa wanafunzi, Mhe Makonda amesema atamwandikia ombi hilo na kulifikisha Rasmi kwa Mhe Lukuvi ili amsaidie kulifikisha kwa Mhe Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa ajili utekekezaji.

No comments:

Post a Comment