
Mwanasiasa mkongwe nchini Tanzania Kingunge Ngombale-Mwiru, 87, amefariki dunia,
Mzee Kingunge amekuwa akitibiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Mwanasiasa huyo mkongwe alilazwa hospitalini mwanzoni mwa Januari akiuguza majeraha ya kushambuliwa na kung'atwa na mbwa nyumbani kwake 22 Desemba mwaka jana na akafanyiwa upasuaji.
Rais John Magufuli amesema apokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha Mzee Kingunge na kusema alikuwa mtu aliyechangia katika juhudi za kupigania uhuru wa Tanzania na na baada ya uhuru awaka mtumishi mtiifu wa chama cha Tanu na baadaye CCM.
"Ametoa mchango mkubwa sana, sisi kama taifa hatuwezi kusahau na tutayaenzi mema yote aliyoyafanya wakati wa utumishi wake uliotukuka," amesema Dkt Magufuli kupitia taarifa.
"Ametuachia somo la kupigania maslahi ya nchi wakati wote, kuwa wazalendo wa kweli, kudumisha Amani na mshikamano, kuchapa kazi kwa juhudi na maarifa na kuwa na nidhamu."
Viongozi pia wametuma salamu zao za rambirambi na kumuomboleza mwanasiasa huyo akiwemo kiongozi wa chama cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe.
Mzee Kingunge alikuwa mmoja wa viongozi wa muda mrefu na miongoni wa watu waliokuwa na ushawishi katika Chama cha Mapinduzi (CCM) hadi alipojiuzulu kutoka kwenye chama hicho Oktoba 2015 akilalamikia alichosema ni ukiukaji wa katiba ya chama hicho.
Kabla ya kujiuzulu, alikuwa amesema kwamba hakuwa amefurahishwa na utaratibu uliotumiwa kumteua mgombea urais wa CCM mjini Dodome Julai mwaka huo.
Hata hivyo, aliahidi kutohamia chama kingine.
Bw Kingunge alikuwa amehduumu katika CCM tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka 1977.
Mke wake, Peras, alifariki dunia mwezi uliopita akitibiwa pia Muhimbili baada ya kulazwa kwa miezi kadha.
Rais wa Tanzania Dkt. John Magufuli alikuwa amefika katika Wodi ya Mwaisela iliyopo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kumjulia hali Mzee Kingunge mwanzoni mwa mwezi Januari.
No comments:
Post a Comment