Wanafunzi wa kiume Z’bar hatarini - TANZA MEDIA ONLINE

Sunday 20 August 2017

Wanafunzi wa kiume Z’bar hatarini

                                                            Kisiwa cha Zanzibar
           
Imeelezwa kuwa jumla ya watoto wa kiume wapatao 40 wanaosoma kati ya darasa la kwanza na la tatu kutoka visiwani Zanzibar wamefanyiwa ukatili wa kuingiliwa kinyume na maumbile.

Hayo yameelezwa na Meneja wa mradi wa elimu ya afya ya uzazi, haki za watoto na vijana, Dk. Ellen Otaru wakati akizungumza na waandishi wa habari katika kongamano la madhimisho ya Vijana Duniani lililofanyika kitaifa mjini Dodoma.

Dk. Otaru amesema kutokana na vitendo vya ukatikili wanavyofanyiwa watoto hao wa kiume kunaweza kuwasababishia madhara makubwa ya kiafya endapo watakosa msaada wa kimatibabu kwa kuwarejesha katika hali yao ya kawaida.

Amesema sababu kubwa ya watoto kufanyiwa vitendo vya kinyama kwa kuingiliwa kinyume na maumbile ni kutokana na kutotolewa kwa elimu ya afya ya uzazi mashuleni.

Dk. Otaru mesema elimu ya afya ya uzazi inatakiwa ianze kutolewa mashuleni kuanzia shule ya awali tofauti na sasa elimu hiyo inaanza kutolewa kuanzia miaka 10 badala ya sita.

Amesema kama elimu ingetolewa mapema ni wazi kuwa watoto wa kiume wangejua mapema kujikinga na watu wenye nia mbaya ya kutaka kuwalawiti huku watoto wa kike wakiwa na maarifa ya kujiepusha na upatikanaji wa ndoa na mimba za utotoni. 

Hata hivyo ameitaja mkoa wa Shinyanga unaongoza kwa tatizo la mimba za utotoni kwa asilimia 53 ukifuatiwa na mkoa wa Tabora na huku akieleza kuwa vitendo hivyo havitokani na umasikini tu bali hata ukosefu wa elimu kwa jamii.

Pia alitoa wito kwa wazazi/walezi kuzungumza na watoto ili kuweza kupata elimu ya afya ya uzazi ambayo itawasaidia na kujua madhara atakayoyapata akitenda jambo hilo badala ya kuwaogopa watoto.

No comments:

Post a Comment